Sunday, August 19, 2012

HONGERA KWA KUOKOKA

  UTANGULIZI
Karibu kwenye Ufalme wa Mungu
Kitabu hiki kimeandikwa kwa ajili yako. Roho Mtakatikfu amekiweka mikononi mwako kwa kusudi muhimu la Mungu ndani ya Kristo.
Katika Jina lile lipitalo majina yote jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu, napenda kukukaribisha katika Ufalme wa Mungu!
Imeandikwa wazi kabisa katika kitabu cha Waefeso 2:19 ya kuwa; “Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu”.
Umepata neema hii ya Mungu, na sasa umeokoka – biblia inakuambia tangu sasa wewe si mgeni wala mpitaji katika Ufalme wa Mungu -  bali wewe ni mwenyeji pamoja na watakatifu wengi waliomo katika nyumba ya Mungu!
Nia ya Roho Mtakatifu kukuwekea kitabu hiki mikononi mwako, ni kukufahamisha angalau kwa kiasi fulani juu ya uamuzi uliofanya wa kutubu dhambi zako, na kumpokea Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wako.
Kitabu hiki kitakusaidia kujua kitu gani kimetokea ulipookoka na mambo muhimu ya kufanya katika maisha hayo mapya ya wokovu.
Umefanya uamuzi wa busara – katika Luka 15:10 biblia inatuambia ya kuwa hata malaika wa mbinguni wanashangilia na kuufurahia uamuzi huo uliofanya.
Na mimi kama mtumishi wa Mungu aliye hai napenda kumshukuru Mungu katika Kristo Yesu kwa kukufunulia siri hii ya wokovu ambayo wengi hawajaiona na wengine wameiona lakini wanaipuzia. Ni maombi yangu kwa Mungu ya kuwa atakutia nguvu na kukupa ufahamu wa rohoni unapokisoma kitabu hiki ili kikusaidie katika maisha yako ya kila siku.
Christopher na Diana Mwakasege ,
S.L.P. 2166,
       ARUSHA           
  UMEFANYA UAMUZI WA BUSARA
            Umefanya uamuzi wa busara. Ndiyo! – tena ni kweli kabisa. Umefanya uamuzi wa busara. Umeamua kutubu dhambi zako kwa Mungu, na kumpokea Yesu Kristo moyoni mwako kama Bwana na Mwokozi wako – umefanya uamuzi wa busara. Naamini pia ya kuwa uamuzi huu uliofanya ni uamuzi wa kudumu.
            Nimeona nikutie moyo namna hii kwa kuwa mtu anapookoka wakati mwingine anasumbuka na mawazo na kujiuliza maswali mengi – akijiuliza ikiwa kwa kuokoka amefanya uamuzi sahihi. Watu wengine kwa kutopata majibu sahihi ya swali hili wanakata tamaa na kurudi nyuma kiroho – na hata wapo wengine wanaoamua kuacha wokovu kabisa.
            Nakutakia heri kwa Bwana na kumwomba Mungu azidi kujifunua wazi zaidi kwako ili usiwe kati ya wale wanaokata tamaa na kuacha wokovu. Umeifanya sala ya toba kwa moyo wako wote na umeokoka – ni uamuzi wa busara mtu yeyote asikudanganye wala kukukatisha tamaa.
Umechagua Baraka!
            Umechagua kuokoka kwa kumwamini na kumpokea Yesu Kristo kama mwokozi wako,maana yake umechagua baraka.
            Inawezekana hukujua lakini mtu ambaye hajaokoka anaishi chini ya laana, na mara anapookoka – Yesu Kristo anamtoa kwenye laana nakumwingiza ndani yake – ambaye ndiye Baraka na chanzo cha baraka zote za Mungu.
            Tangu zamani Mungu alimpa mtu uhuru wa kuchagua kati ya baraka na laana aliposema           
“ Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana; baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana Mungu wenu…. Na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya Bwana…. (Kumbukumbu la Torati 11:26-28)
            Umechagua kuokoka – umechagua baraka! Baraka maana yake, furaha, amani, kufanikiwa, kustawi, kukua,kunawiri na kunona!
            Ndiyo maana Mtume Paulo aliandika katika kitabu cha Waefeso 1:3 hivi, “Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo.”
            Huu mstari unazungumza juu yako pia kwa kuwa unapookoka unaingia “ndani yake Kristo”. Kwa kuwa ulipookoka uliingia ndani yake Kristo, kwa hiyo umebarikiwa kwa baraka zote za rohoni!
            Unaweza ukajiuliza kama ni baraka zote za rohoni je za kimwili na za akili nitazipataje? Fahamu neno hili baraka zote zimeanza rohoni!
            Ndiyo maana imeandikwa hivi katika kitabu cha Wagalatia 3:13, 14 kuwa; “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu, maana imeandikwa amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti, ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya roho kwa njia ya amani”

No comments:

Post a Comment

mwakasege A moment of worship

ushuhuda