Monday, August 20, 2012

KWA NINI BWANA YESU ALITUOMBEA UMOJA?

Wiki ya Kwanza

UTANGULIZI

            Mungu tunayemwamini katika Yesu Kristo, ni Mungu wa mipango na makusudi kamili. Tangu vizazi na vizazi tabia hii ya Baba yetu, imejidhihirisha wazi.
            Baba yetu huyu, ambaye pia, ni Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, hawezi kufanya kitu au kusema kitu, bila ya kuwa na sababu.
            Mungu aliumba dunia hii, kwa kusudi kamili, ili ikaliwe na watu isiwe tupu.
            Mungu aliumba jua, mwezi, sayari na nyota mbali mbali, kwa makusudi kamili, ili viwe ndiyo dalili za majira na siku na miaka na tena iwe ndiyo mianga katika anga la mbingu itie nuru juu ya nchi.
            Mungu alimtokea Musa katika kijiti kilichokuwa kikiwaka moto, kwa kusudi kamili, ili apate kuwatoa watu wake, wana wa Israeli kutoka Misri.
            Mungu alimtoa Mwana wake wa pekee Yesu Kristo, kwa kusudi kamili, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.
Mungu alimwaga Roho wake Mtakatifu juu ya watu wake, kwa kusudi kamili, ili wapate nguvu ya kuwawezesha kuwa mashahidi wa Kristo katika ulimwengu mzima.
  Ni kweli kabisa ya kwamba, Mungu tunayemwamini katika Yesu Kristo, ni Mungu wa mipango na makusudi kamili. Hafanyi kitu bila ya kuwa na sababu nacho.
Kwa hiyo alipokuwa akisema na watumishi wake, alikuwa na kusudi na ujumbe kamili kwa ajili ya watu wake.
 Na aliponiita kwenye utumishi wake alikuwa na mipango na makusudi kamili kwa ajili ya watu wake. Kwa hiyo niliposikia sauti yake ndani ya roho yangu nilipokuwa kwenye mkutano wa ‘Easter Crusade’, Tukuyu, Mbeya Aprili 1987, nilijua hakika ya kuwa kuna jambo la muhimu.
Nilisikia sauti ya Bwana ndani ya roho yangu ikisema; “NATAKA KUSEMA NA WATU WANGU”.
Si kwamba nilisikia sauti kama ya mtu akiongea; hapana; bali kwa uwezo wa Roho wake Mtakatifu, nilisikia sauti hiyo ndani ya roho yangu. Na nilijua hakika ya kuwa hiyo ni sauti ya Bwana wangu na Mwokozi wangu. Hata Yeye alisema kuwa ndiye pekee aliye mchungaji mwema, walio wake anawajua, na wao wanamjua, na sauti yake wanaijua (Yohana 10:1-6).
Mkutano huo wa kiroho ulikuwa umejumuisha watu wa Mikoa mbali mbali na pia watu wa madhehebu mbali mbali. Na Bwana aliposema nami kwamba anataka kusema na watu wake ilikuwa ni mchana wa siku ya pili ya mkutano.
Kwa hiyo baada ya kusikia hivyo, nilitafuta mahali pa faragha katika chumba kimoja; nikapiga magoti, na nikawa tayari kusikia lile ambalo Bwana alikuwa anataka lisikike kwa watu wake.
Maneno aliyoniambia yalihusu juu ya UMOJA WA WATU WAKE. Na waliokuwapo kwenye mkutano huo walipata nafasi ya kusikia kwa muhtasari tu, juu ya Umoja wa watu wa Mungu.
Maneno hayo ya Bwana  juu ya umoja wetu ni muhimu sana. Na kwa ajili hiyo, Roho wa Bwana ameniongoza kuyaandika kwa undani zaidi, ili watu wengi waweze kuyapata na kuyafanyia kazi.
Jambo ambalo Bwana analiona katikati yetu, katikati ya wakristo, ni kukosa Umoja wa kweli. Na jambo hili linamhuzunisha sana Mungu. Hii ni kwa sababu watu wake ndiyo mwili wake (1Wakorintho 12:27). Kwa hiyo kukiwa na nyufa katika uhusiano wa mkristo na mkristo mwingine, maana yake mwili wake umepata nyufa.
Kusudi lake kubwa la kutulinda, kututunza, kutulisha, kututakasa na kutuongoza ni ili atulete mbele za Baba yetu aliye mbinguni, bila waa na wala kunyanzi.
Lakini, hali inayoonekana sasa ni ya kusikitisha. ‘Fellowships’ nyingi hazina umoja na zimetawaliwa na mafarakano. Viongozi wa Kanisa nao pia hawana umoja kila mmoja anafanya mambo yake mwenyewe, ambayo anayaona ni bora kuliko ya mwenzake. Vikundi vingi vya huduma za kikristo havina umoja wa kweli.
Yesu Kristo alituombea umoja. Je! Maombi yake yamejibiwa au bado? Na alikuwa na sababu gani alipokuwa anatuombea? Je! Yesu Kristo alikuwa na mpango wowote aliouandaa juu ya umoja wa mwili wake, ambalo ni Kanisa?
Ni nini chanzo cha mafarakano na kukosa umoja katikati ya watu wa Mungu? Tufanye nini ili tupate kusimama katika umoja wa kweli?
 Maswali hayo na mengine yanajibiwa katika somo hili.
            Sasa, ngoja niseme jambo moja muhimu:
Mungu huyu tunayemtumika ni Mungu aliye na kusudi kamili, katika kila jambo analolifanya na kulisema. Na kwa mtazamo huu, nakuambia hivi, Mungu ameweka maandiko ya somo hili mikononi mwako kwa kusudi kamili, kwa ajili ya utukufu wa Jina lake Takatifu.
Kwanza:           Kwa sababu anakupenda upeo, hapendi   upotee.
Pili:                  Kwa sababu wewe ni kiungo cha mwili wake, ambao ndilo Kanisa
Tatu:                Kwa sababu anataka uhusike moja kwa moja katika kushirikiana na Roho wake Mtakatifu, ili kuwashirikisha wengine ujumbe huu.
Ni maombi yangu kwa Mungu katika Jina la Yesu Kristo aliye hai, ya kuwa Roho wake akutie nuru katika utu wako wa ndani upate kuyaelewa yote na kuyafanyia kazi ipasavyo. Na ukiishayasoma uwashirikishe wengine bila kuyapindua pindua.
Hizi ni siku za mwisho, na tunatakiwa tuwe waangalifu katika yote tunayoyasikia au kuyasoma. Tunatakiwa tuyachambue, na kuyapima, halafu tuyachukue yaliyo mema yanayotujenga pamoja na siyo kutubomoa.
Kwa hiyo nakushauri, katika Jina la Yesu Kristo, ya kwamba unapoyasoma yaliyomo humu, uwe na BIBLIA yako karibu upate kuifuatilia mistari yote niliyoinukulu. Bwana na akuwezeshe kuyatafakari na kuyafanyia kazi ili wote tuwe na Umoja kama Baba na Kristo walivyo umoja.
Sifa na Utukufu na uweza, na nguvu vina Mungu wetu katika Kristo Yesu, milele na milele – Amina.
YESU KRISTO ALIOMBA UMOJA KWA AJILI YA NANI?
Neno Umoja maana yake nini?
Yesu Kristo alipokuwa anaomba juu ya Umoja kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Yohana sura ya kumi na Saba, alilitumia neno Umoja mara tano.
Neno Umoja linaweza kuwa na maana mbali mbali, kutokana hasa na mtu anayelitumia, mahali anapolitumia na kwa ajili ya kitu gani.
Neno Umoja likitumika kwa ajili ya watu lina maana ya patana, afikiana, elewana na lingana, katika roho, na nia, mawazo, maneno  na matendo.
Yesu Kristo alipokuwa akitumia neno Umoja, alikuwa anamaanisha hao anaowaombea wapatane, waafikiane, waelewane, na walingane katika roho zao, nia zao, mawazo yao, maneno na matendo yao.
Sasa, hili si jambo dogo!
Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani, akiwa amevaa mwili wa kibinadamu; kabla ya kufa na kufufuka; aliomba maombi ya namna nyingi.
Na mojawapo ya maombi yake kwa Baba Mungu, yalikuwa juu ya Umoja wetu.
“Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao. Wote wawe na Umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja. Mimi ndani yao; nawe ndani yangu, ili wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma, ukawapenda wao kama ulivyonipenda mimi (Yohana 17:20 – 23).

Sunday, August 19, 2012

FAHAMU UWEZO WA DAMU YA YESU KRISTO

                Siku moja usiku nikiwa katika chumba cha hoteli moja hapa hapa nchini, baada ya kutoka kwenye semina ya kiroho; Roho Mtakatifu alisema ndani ya roho yangu kuwa; “Fundisha juu ya Damu ya Yesu Kristo”.
                Tangu wakati huo nimekuwa na maombi ya mara kwa mara, nikiomba Roho Mtakatifu anifundishe juu ya Damu ya Yesu Kristo. Nimekuwa nikisoma na kutafakari neno la Mungu linalofundisha juu ya damu ya Yesu Kristo. Ni muda umepita sasa tangu nipate agizo hili. Ndani ya moyo wangu naona ya kuwa muda umefika wa mimi kuanza kuwashirikisha wenzangu yale ambayo tayari yamo ndani yangu ingawa ni machache, juu ya Damu ya Yesu Kristo.
                Katika mfulilizo wa somo hili,tutashirikiana juu ya mambo manne tunayopata katika Damu ya Yesu Kristo. Ukweli ni kwamba katika damu ya Yesu Kristo kunapatikana zaidi ya mambo manne nitakayokushirikisha humu; lakini kwa sasa naona nianze na haya manne:-
1.       Uwezo wa Damu ya Yesu Kristo katika kuondoa dhambi. Imeandikwa katika kitabu cha 1Yohana 1:9 kuwa; “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata ATUONDOLEE dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote”.
2.       Uwezo wa Damu ya Yesu Kristo katika kupatanisha. Imeandikwa katika kitabu cha Waefeso 2:13-16 kuwa; “Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo. Kwa maana yeye ndiye amanin yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga. Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu  mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani. AKAWAPATANISHA wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba”
3.       Uzima wa Milele katika Damu ya Yesu Kristo. Imeandikwa katika kitabu cha Yohana 6:53-54 kuwa; “Basi Yesu akawaambia Amini, amini, nawaambieni, msipoula mwili wake mwana wa Adamu nakuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao UZIMA WA MILELE…..”
4.       Uwezo wa Damu ya Yesu Kristo katika kutulinda. Imeandikwa katika kitabu cha ufunuo wa Yohana 12:11a kuwa; “Nao wakamshinda (shetani) kwa damu ya mwana-Kondoo….”
Mtihani mkubwa sana kwetu sisi wakristo ni kuyaweka katika matendo yale tunayofahamu katika Biblia. Nakushauri kwa Jina la Yesu Kristo kuwa uwe mtendaji wa neno, na usiwe msomaji tu.
Ni maombi yangu kwa Bwana ya kuwa Roho wa ufahamu wa Bwana atakuwa juu yako unaposoma na kutenda unayofundishwa katika kitabu hiki.

UWEZA WA JINA LA YESU

Mtume Paulo anasema katika Waraka wake kwa Wakolosai sura ya tatu na mstari wa kumi na saba kuwa; “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika JINA LA BWANA YESU, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.”
            Hii ina maana ya kuwa, tukila tule katika Jina la Yesu Kristo. Tukilala tulale katika Jina la Yesu Kristo. Tukizungumza tuzungumze katika jina la Yesu Kristo. Tukiimba tuimbe katika jina la Yesu Kristo. Tukitembea tutembee katika jina la Yesu Kristo. Tukisafiri tusafiri katika jina la Yesu Kristo. Tukilima shambani tulime katika jina la Yesu Kristo; na kadhalika.
            Kwa nini tunatakiwa tufanye mambo yote katika jina la Yesu Kristo? Jina hili la Yesu Kristo lina sehemu gani katika maisha yetu ya kila siku?
Kama tunatakiwa kufanya mambo yote katika jina la Yesu Kristo, kwa nini hatufanyi hivyo?
Ukitafakari maagizo tuliyopewa katika biblia utaona ya kuwa, maisha yetu yote yanalitegemea jina hili la Yesu Kristo.
Kama mambo yetu yote yanatakiwa yafanyike kwa jina la Yesu, basi ni muhimu tujifunze zaidi na zaidi kila siku juu ya jina hili la ajabu.
Ni maombi yangu kwa Mungu Baba, katika jina la Yesu Kristo ya kuwa maneno yaliyomo katika somo hili yatachochea kwa upya kiu iliyomo ndani yako ya kutaka kufahamu zaidi siri iliyomo ndani ya jina la Yesu Kristo.
Uweza wa Jina la Yesu / Utang / 1 / 2 / 3 / 4 / 5 / 6 /

JIFUNZE KUSAMEHE NA KUSAHAU

            Tuna uhakika ya kwamba, Roho Mtakatifu anakuongoza kusoma somo hili kwa makusudi kamili.

            Maneno yaliyomo humu ni ya kukusaidia wewe na Wakristo wote, ili tuweze kuishi maisha ya "amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao."(Waebrania 12:14).
            Kusamehe na kusahau ni tatizo kubwa ambalo limewazuia wakristo wengi wasipokee majibu ya maombi yao toka kwa Mungu. Ninaamini kuwa maneno yaliyomo humu yatakusaidia katika kupokea majibu ya maombi mengi ambayo hujayapokea.
            Ni maombi yetu kwa Mungu, katika Jina la Yesu Kristo ya kwamba, Roho Mtakatifu ayachukue mafundisho haya na kuyaandika katika moyo wako, na akusaidie kuyatenda.
            Na unaposoma itakuwa ni vizuri ukiwa na Biblia yako karibu, ili usome mistari yote tuliyoiandika. Somo hili tutajifunza kwa wiki sita mfululizo. Somo la wiki inayofuata litakuwa linajenga juu ya somo la wiki linalotangulia hasa baada ya wiki ya kwanza.
 Tutakuwekea mfululizo wa somo hili kama ifuatavyo:
Wiki ya Kwanza: Kutosamehe ni kikwazo
Wiki ya Pili: Tabia ya Mungu ya kusamehe ndani yako
Wiki ya Tatu: Hasara za kulipiza kisasi
Wiki ya Nne: Hatua Tano Muhimu katika kusamehe
Wiki ya Tano: Je! aliyekukosea asipokuomba msamaha ufanyeje?
Wiki ya Sita: Utajuaje kama bado hujasamehe?

            Tunataraji ya kuwa utaungana pamoja nasi kila wiki katika kujifunza somo hili. Ni maombi yetu kwa Mungu ya kuwa somo hili litakusogeza hatua nyingine muhimu katika maisha yako.
Jifunze kusamehe na kusahau / Utang / 1 / 2 / 3 / 4 / 5 / 6

HONGERA KWA KUOKOKA

  UTANGULIZI
Karibu kwenye Ufalme wa Mungu
Kitabu hiki kimeandikwa kwa ajili yako. Roho Mtakatikfu amekiweka mikononi mwako kwa kusudi muhimu la Mungu ndani ya Kristo.
Katika Jina lile lipitalo majina yote jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu, napenda kukukaribisha katika Ufalme wa Mungu!
Imeandikwa wazi kabisa katika kitabu cha Waefeso 2:19 ya kuwa; “Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu”.
Umepata neema hii ya Mungu, na sasa umeokoka – biblia inakuambia tangu sasa wewe si mgeni wala mpitaji katika Ufalme wa Mungu -  bali wewe ni mwenyeji pamoja na watakatifu wengi waliomo katika nyumba ya Mungu!
Nia ya Roho Mtakatifu kukuwekea kitabu hiki mikononi mwako, ni kukufahamisha angalau kwa kiasi fulani juu ya uamuzi uliofanya wa kutubu dhambi zako, na kumpokea Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wako.
Kitabu hiki kitakusaidia kujua kitu gani kimetokea ulipookoka na mambo muhimu ya kufanya katika maisha hayo mapya ya wokovu.
Umefanya uamuzi wa busara – katika Luka 15:10 biblia inatuambia ya kuwa hata malaika wa mbinguni wanashangilia na kuufurahia uamuzi huo uliofanya.
Na mimi kama mtumishi wa Mungu aliye hai napenda kumshukuru Mungu katika Kristo Yesu kwa kukufunulia siri hii ya wokovu ambayo wengi hawajaiona na wengine wameiona lakini wanaipuzia. Ni maombi yangu kwa Mungu ya kuwa atakutia nguvu na kukupa ufahamu wa rohoni unapokisoma kitabu hiki ili kikusaidie katika maisha yako ya kila siku.
Christopher na Diana Mwakasege ,
S.L.P. 2166,
       ARUSHA           
  UMEFANYA UAMUZI WA BUSARA
            Umefanya uamuzi wa busara. Ndiyo! – tena ni kweli kabisa. Umefanya uamuzi wa busara. Umeamua kutubu dhambi zako kwa Mungu, na kumpokea Yesu Kristo moyoni mwako kama Bwana na Mwokozi wako – umefanya uamuzi wa busara. Naamini pia ya kuwa uamuzi huu uliofanya ni uamuzi wa kudumu.
            Nimeona nikutie moyo namna hii kwa kuwa mtu anapookoka wakati mwingine anasumbuka na mawazo na kujiuliza maswali mengi – akijiuliza ikiwa kwa kuokoka amefanya uamuzi sahihi. Watu wengine kwa kutopata majibu sahihi ya swali hili wanakata tamaa na kurudi nyuma kiroho – na hata wapo wengine wanaoamua kuacha wokovu kabisa.
            Nakutakia heri kwa Bwana na kumwomba Mungu azidi kujifunua wazi zaidi kwako ili usiwe kati ya wale wanaokata tamaa na kuacha wokovu. Umeifanya sala ya toba kwa moyo wako wote na umeokoka – ni uamuzi wa busara mtu yeyote asikudanganye wala kukukatisha tamaa.
Umechagua Baraka!
            Umechagua kuokoka kwa kumwamini na kumpokea Yesu Kristo kama mwokozi wako,maana yake umechagua baraka.
            Inawezekana hukujua lakini mtu ambaye hajaokoka anaishi chini ya laana, na mara anapookoka – Yesu Kristo anamtoa kwenye laana nakumwingiza ndani yake – ambaye ndiye Baraka na chanzo cha baraka zote za Mungu.
            Tangu zamani Mungu alimpa mtu uhuru wa kuchagua kati ya baraka na laana aliposema           
“ Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana; baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana Mungu wenu…. Na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya Bwana…. (Kumbukumbu la Torati 11:26-28)
            Umechagua kuokoka – umechagua baraka! Baraka maana yake, furaha, amani, kufanikiwa, kustawi, kukua,kunawiri na kunona!
            Ndiyo maana Mtume Paulo aliandika katika kitabu cha Waefeso 1:3 hivi, “Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo.”
            Huu mstari unazungumza juu yako pia kwa kuwa unapookoka unaingia “ndani yake Kristo”. Kwa kuwa ulipookoka uliingia ndani yake Kristo, kwa hiyo umebarikiwa kwa baraka zote za rohoni!
            Unaweza ukajiuliza kama ni baraka zote za rohoni je za kimwili na za akili nitazipataje? Fahamu neno hili baraka zote zimeanza rohoni!
            Ndiyo maana imeandikwa hivi katika kitabu cha Wagalatia 3:13, 14 kuwa; “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu, maana imeandikwa amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti, ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya roho kwa njia ya amani”

mwakasege A moment of worship

ushuhuda